MWONGOZO WA KISASA WA UFUGAJI WA KUKU


UTANGULIZI

Kuku ni mifugo kama ilivyo mifugo mingine. kuku wamezoeleka kwani hufugwa na watu wengi barani Afrika na kwingineko. Hata hivyo ni watu wachache sana wanao tambua thamani ya kuku.

Nchini Tanzania watu walio na kuku ni wengi japo inasadikika kuwa ni asilimia 8.2 tu kati ya wote walio na kuku wanao nufaika kwa sehemu na umiliki wa kuku. Utafiti umeonesha kuwa Watanzania wengi wanamiliki kuku, siyo wafugaji wa kuku kwani kuku wao hujifuga wenyewe. Hii ni kutokana na wengi kati ya wafugaji kufuga kwa mazoea.

Ufugaji wa kuku ukifanyika kwa utaratibu mzuri huleta mafanikio makubwa kwa mfugaji. Hauishii kumuwezesha kuishi, bali humtajirisha na kumuweka katika hatua ya mafanikio zaidi kwa kadri ya juhudi zake. Ufugaji wa kuku ni fursa pana inayo weza kutekelezwa na yeyote bila kujali mtaji wake, elimu, mazingira alipo wala hali yake ya kimaisha. Ufugaji wa kuku kibiashara haujawahi kumuangusha yeyote aliye thubutu kuutekeleza kwa malengo na kuendesha kwa ufanisi.

Kitabu hiki ni mwongozo sahihi wa namna ya kunufaika na ufugaji wa kuku. Kimebainisha mfumo rahisi na wa kisasa wenye mafanikio makubwa katika ufugaji wa kuku. Changamoto zote zinazo ukabiri ufugaji wa kuku zimetatuliwa katika kitabu hiki. Anza kuyafuata maelekezo yake, unufaike na kutajirika kupitia ufugaji wa kuku.

YALIYOMO

UTANGULIZI 2

YALIYOMO.. 3

SURA YA 1. 4

MRADI WA UFUGAJI WA KUKU.. 4

MAZAO YA KUKU.. 5

AINA ZA KUKU.. 5

SURA YA 2. 6

KUKU WA ASILI 6

SIFA ZA KUKU WA ASILI 6

AINA ZA KUKU WA ASILI 6

FAIDA ZA KUFUKA KUKU WA ASILI 8

UFUGAJI WA KUKU WA ASILI 8

MIFUMO YA UFUGAJI WA KUKU WA ASILI 8

MAHITAJI MUHIMU KATIKA UFUGAJI WA KUKU WA ASILI 11

HATUA ZA UFUGAJI WA KUKU WA ASILI KWA FAIDA. 11

KUCHAGUA KUKU BORA WA KUFUGA. 11

BANDA BORA LA KUFUGIA. 12

UJENZI WA BANDA. 13

KUTUNZA NA KULISHA KUKU KULINGANA NA HATUA MBALIMBALI ZA UKUAJI 14

KULEA VIFARANGA. 16

ULISHAJI WA KUKU.. 18

USAFI KATIKA BANDA LA KUKU.. 21

SURA YA 3. 22

KUKU WA KISASA. 22

KUKU WA MAYAI 22

KUKU WA NYAMA. 22

Tofauti kati ya kuku wa Asili na kuku wa Kisasa. 23

HATUA ZA KUFUKA KUKU WA KISASA. 23

SURA YA 4. 25

UFUGAJI WA KUKU WA MAYAI 25

Utumiaji wa mashine; 25

MATAYARISHO KABLA YA VIFARANGA KUWASILI 26

UAGIZAJI WA VIFARANGA. 27

MAPOKEZI YA VIFARANGA. 27

ULISHAJI 28

JOTO.. 28

MALEZI YA MITEMBA NA MITETEA. 29

MATUNZO YA KUKU WAZAZI 31

SURA YA 5. 33

UFUGAJI WA KUKU WA NYAMA. 33

KUFUKA KWA FAIDA HUHITAJI KUZINGATIA HAYA. 33

SURA YA 6. 35

MAGONJWA YA KUKU, KINGA NA TIBA ZAKE. 35

MAGONJWA YA KUKU, KINGA NA TIBA ZAKE KITAALAM.. 36

FAHAMU BAADHI YA MAGONJWA HATARI YASHAMBULIAYO KUKU, UENEAJI WAKE, DALILI, KINGA NA TIBA ZAKE: 37

Sura ya 7. 50

UTENGENEZAJI WA CHAKULA CHA KUKU. 50

SURA YA 1

MRADI WA UFUGAJI WA KUKU

Nyama ya kuku pamoja na mayai ni hitaji kubwa kote duniani. Nchini Tanzania kunasadikika kuwa kuna kuku wapatao milioni therathini na nne ambao ni wachache ukilinganisha na mahitaji yaliyopo. Kwa mujibu wa shirika la chakula duniani “FAO” mahitaji ya nyama ya kuku kwa mtu mmoja ni kilo 6.8 kwa mwaka ambapo Nchini Tanzania utafiti unaonesha kuwa matumizi ya nyama ya kuku yaliyopo kwa sasa ni wastani wa kilo 0.7 kwa kila mtu kwa mwaka. Hapa utagundua kuwa bado uhitaji wa nyama ya kuku uliopo ni mkubwa kwani kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012, Watanzania ni zaidi ya million 44. Kwa sababu hiyo ufugaji wa kuku ni fursa pana sana hapa Nchini.

Idadi ya wafugaji wa kuku nchi Tanzania ni wengi ambao kimsingi kama wangefuga kwa kuzingatia taratibu za ufugaji, wangelisha kuku siyo Tanzania tu bali wangelisha Dunia. Hatahivyo ufugaji wao ni duni kwani wengi wao wamekuwa wakifuga kwa mazoea. Wanao kuku majumbani mwao lakini hawawajali wala kuwapa nafasi yoyote ya umuhimu kwa upande wa huduma. Hii imepelekea ufugaji wa kuku kuonenaka kuwa ni jambo la kawaida ingawa kwa uhalisia wake ufugaji wa kuku ni mradi, ni kazi, ni ajira na ni maisha kamili ya watu.

Mradi wa ufugaji wa kuku una utajiri mkubwa ukifanyika kwa ufanisi. Huhitaji elimu kiasi katika utekelezaji wake, nguvu kiasi na muda wa kutosha. Ni rahisi, unao weza kufanywa na mtu yeyote. Ufugaji wa kuku ni nyenzo muhimu katika kupambana na wimbi la umaskini. Pamoja na soko la uhakika, bado ufugaji kuku haujatumika ipasavyo kupambana na umaskini unao wakabiri Watanzania wengi. Kuku wa kienyeji ambao hufugwa na watu wengi wamekuwa wakifugwa bila kupatiwa mahitaji muhimu kama chakula cha ziada, makazi bora, kinga na tiba za magonjwa pamoja na uangalizi! Hali inayo pelekea wafugaji kunufaika na kitoweo tu pamoja na kipato kidogo katika kazi yao ya ufugaji.

MAZAO YA KUKU

Faida ya kufuga kuku inapatikana katika mazao ya kuku. Mazao ya kuku huweza kumnufaisha mfugaji kwa kuyatumia mwenyewe pia kuuza na kujipatia pesa.

Mazao yatokanayo na kuku ni;

  • Nyama ya kuku.
  • Mayai.
  • Manyoya.
  • Mbolea n.k.

AINA ZA KUKU

Yapo makundi makuu mawili ya kuku; Kuku Wa asili na kuku wa kisasa. katika makundi haya ndimo tunamo pata aina mbalimbali za kuku. Uwepo wa aina za kuku hutokana na muingiliano wa vinasaba pamoja uendelezaji wa kibaiolojia. Katika kuendeleza kuku kibailojia; Wataalamu wa Baiolojia hukutanisha kuku wa aina moja na wa aina nyingine, kutumia vyakula au dawa ili kupata aina bora kulingana na malengo yao. Wataalamu hawa hufanya hivi kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa mazao ya kuku hivyo juhudi yao ni kuhakikisha wanapata kuku wanao taga kwa haraka na wanao taga mayai mengi.

SURA YA 2

KUKU WA ASILI

Kwa namna nyingine huitwa kuku wa kienyeji. Hawa ni kuku wa asili ambao walikuwepo kabla ya kuanza kwa uedelezaji wa ki-baiolojia/teknilojia na upandikizaji wa mbegu. Ni kuku ambao bado wapo katika asili yao. Ni Wastahimivu wa changamoto za kimazingira ikiwa ni pamoja na magonjwa, pia huweza kujihudumia kiasi fulani ikiwa ni pamoja na kujitafutia chakula, kujilinda n.k. Hata hivyo kwa lengo la kuwafuga kwa faida, mfugaji anatakiwa kuwafuga kiaalam na kuwapa huduma zote muhimu ili kunufaika na kazi yake ya ufugaji.

SIFA ZA KUKU WA ASILI

  • Wana uwezo wa kujitafutia chakula.
  • Ni wastahimivu wa magonjwa.
  • Wana uwezo wa kuatamia mayai, kutotoa na kulea vifaranga.
  • Ni wastahimivu wa mazingira na hali ya hewa kama ukame, baridi n.k.
  • Nyama na mayai yake vina ladha nzuri na ni nzuris zaidi katika afya.
  • Kwa kiasi fulani wana uwezo wa kujiilinda na maadui kama vile; mwewe, kunguru, vicheche, kenge n.k

Kuku wa kienyeji wanazo sifa nyingi nzuri lakini pammoja na sifa hizo, ukihitaji kuwafuga kwa faida, ni muhimu wapewe huduma bora wanayostahili ikiwa ni pamoja na chakula cha kutosha.

AINA ZA KUKU WA ASILI

Ili kufanikisha kusudi la kufuga kuku kwa faida, hatua ya kwanza kabisa ya kuzingatia ni kuchagua aina bora ya kuku wa kufuga. Aina za kuku wa asili wanao patikana Tanzania hutambulika kutokana na tofauti za kimaumbile pamoja na eneo kuku huyo analo toka. Kuku wa kienyeji/asili wapo wa aina nyingi ikiwa ni pamoja na;

  • Umbo kati.
  • Kibutu.
  • Nungunungu/ Njachama
  • Kishingo
  • Ching’wekwe
  • Singamagazi
  • Kibwezi n.k.

Umbo kati; kuku hawa ndio walio zoeleka hasa kuitwa kuku wa kienyeji (wa kawaida). Jogoo huwa na wastani wa uzito wa kilo 1.8 huku tetea wakiwa na wastani wa kilo 1. Mayai yake yana wastani wa gram 43. Kuku hawa hupatikana sehemu zote Nchini na rangi ya manyoya yao ni mchanganyiko. Kuku hawa hukua upesi na pia hupata kinga upesi baada ya kuchanjwa.

Kuchi; ni kuku wakubwa, warefu. Hutambulika kwa kusimama mgongo ukiwa wima. Wana manyoya machache mwilini, hasa kifuani. Wana mdomo mfupi na vilemba vyao ni vidogo. Jogoo la kuchi huwa na wastani wa uzito wa kilo 3.5 na tetea kilo 2. Mayai ya kuchi yana uzito wa wastani wa gram 45. Ni wazuri sana kwa nyama.

Kibutu; hawa ni kuku wenye mkia mfupi. Manyoya yao ya mkiani ni mafupi na yameinama kuelekea chini.

Njachama; ni aina ya kuku wa asili ambayo wengine huiita Nungunungu. hawa ni kuku wenye manyoya yaliyosimama.

Kishingo; hawana manyoya shingoni.

Singamagazi; kuku hawa hutambulishwa na rangi zao. Majogoo huwa na rangi ya moto na matetea huwa na rangi ya nyuki. Ni aina ya kuku wa asili wanao patikana zaidi maeneo ya Tabora. Jogoo huwa na uzito wa wastani wa kilo 2.9 na tetea kilo 2 huku mayai yakiwa na wastani wa gram 56. Kuku hawa ni mbegu nzuri kwa uzarishaji wa mayai na nyama.

Ching’wekwe; kuku hawa wana umbo dogo na uzito mdogo wa wastani wa kilo 1.5 kwa jogoo na kilo 1 kwa tetea. Mayai yake huwa na uzito wa gram 37. Wana sifa ya kutaga mayai mengi kuliko kuku wengine wa kienyeji wanao patikana Tanzania. Kwa kiasi kikubwa hupatikana umasaini pamoja na maeneo ya Chakwale mkoani Morogoro

Kibwezi; wana manyoya mengi kichwani.

Aina zingine ni kama vile; Mbeya, Unguja, kuku aina ya Pemba n.k.

FAIDA ZA KUFUKA KUKU WA ASILI

  • Kuku wa kienyeji ni chanzo rahisi cha pesa, hivyo hukuza kipato na kuondoa umaskini.
  • Kupata kitoweo.
  • Nyama na mayai ya kuku wa kienyeji ni chanzo kizuri cha protini mwilini.
  • Kinyesi chake ni mbolea.
  • Maganda ya mayai yake hutumika kutengeneza mapambo na wengine hutumia kama dawa kujitibu magonjwa kadha wa kadha.
  • Manyoya yake hutumika kutengeneza mapambo na mito ya kulalia pamoja na mito ya kukalia.
  • Majogoo ya asili hutumika kutambua muda na wakati mwingine kama alamu ya kukuamsha asubuhi.
  • Husaidia kupunguza wadudu hatari kama Nge, n.k, pia hutumika kugundua wanyama hatari kama Nyoka, n.k katika mazingira ya nyumbani.
  • Kuendeleza kizazi cha kuku wa asili hapa Nchini.
  • Ufugaji wa kuku ni fursa ya kujiajiri na kuajiri.
  • Kuku hutumika katika shughuri za utafiti hasa utafiti wa kibailojia.

UFUGAJI WA KUKU WA ASILI

Kumiliki kuku wa asili ni suala linalo jitegemea na kuwafuga ni suala lingine. Mfugaji ni msimamizi na mwangalizi, hivyo ufugaji ni usimamizi na uangalizi. Mfugaji kama msimamizi anatakiwa kutumia muda wote, pia mfugaji kama mwangalizi anatakiwa kuhakikisha mifugo yake inakata huduma stahili na mahitaji yote muhimu kwa wakati na mazingira sahihi.

MIFUMO YA UFUGAJI WA KUKU WA ASILI

Ufugaji upo wa aina mbalimbali. Mifumo ya ufugaji unao tumika sana hapa Tanzania ni;

i. Ufugaji huria; unaweza kuuita ufugaji usio jali. Katika ufugaji huria kuku huachwa kujitafutia mwenyewe chakula na maji, mfugaji hawajibiki kuwapatia chakula cha ziada na ikitokea ni mara chache sana. Kuku hulala eneo lisilo rasmi, kulala jikoni, kwenye kibanda au ndani kwa mfugaji n.k njia hii ni njia rahisi ambayo hutumika sana kufuga kuku wa kienyeji na huhitaji eneo kubwa litakalo tosha kuku kutembea ili kujitafutia chakula.

Faida zake;

  • Kuku hupata chakula mchanganyiko ambacho kinawafaa kiafya.
  • Kuku hupata hewa, joto na mwanga wa jua wa kutosha.
  • Ni njia rahisi ya kufuga.
  • Hutumia gharama ndogo katika kufuga, n.k

Hasara zake;

  • Usalama wa kuku siyo wa uhakika hivyo wanaweza kuibiwa ama kudhuliwa na wanyama au kukumbwa na tatizo kwa namna yoyote.
  • Uharibu mazingira kama kula na mimea ya bustanini mazao kama nafaka, n.k.
  • Matunda yake ni madogo kiasi kwamba hawanufaishi vizuri mfugaji. Na Ni rahisi kuambukizwa magonjwa.

Zingatia;

  • Mfumo huu wa ufugaji ni rahisi lakini siyo rafiki kwa mfugaji mwenye malengo ya kufanikiwa.

ii. Nusu huria; Katika mfumo huu kuku hujengewa banda na kuzungushiwa wigo (uzio) kuzunguka banda. Kuku hulala kwenye banda nyakati za usiku na kushinda ndani ya uzio wakati wa mchana wakila chakula na maji humo. Nusu huria ni mfumo ambao huonesha sehemu kubwa ya mafanikio kwa mfugaji.

Faida zake;

  • Utunzaji wa kuku ni rahisi ukilinganisha na mfumo huria.
  • Kuku wanakuwa salama ukilinganisha na mfumo huria.
  • Ni rahisi kudhibiti ukusanyaji wa mayai.
  • Ukuaji wa kuku ni mzuri maana hupata chakula cha ziada.
  • Ufugaji wa nusu huria huhitaji sehemu ndogo ya kufugia ukilinganisha na huria.
  • Ni rahisi kuweka kumbukumbu.

Hasara zake;

  • Gharama kiasi huongezeka katika ufugaji ukiliganisha na mfumo huria.
  • Ugonjwa ukiingia, ni rahisi kuenea haraka.
  • Matumizi ya muda mrefu ya eneo husika laweza kuwa na minyoo au vimelea vingine vya magonjwa.

Zingatia;

  • Mfumo huu ni mzuri kwa ufugaji ila huhitaji usafi. Eneo husika lifanyiwe usafi kila siku na ikiwezekana kuwa na mzunguko wa kubadilisha eneo la kufugia angalau kila mwaka iwapo inawezekana.

iii. Shadidi; Shadidi ni mfumo wa kufugia ndani ya banda tu. Katika mfumo huu kuku hujengewa banda rasmi na hufugwa wakiwa ndani ya banda huku wakipatiwa chakula, maji na kupewa huduma zingine zote muhimu humohumo bandani maisha yao yote. Mara nyingi mfumo huu hutumika kufugia kuku wa kisasa lakini ni mzuri pia katika ufugaji wa kuku wa asili. Sakafu ya banda la kutumia katika ufugaji shadidi ifunikwe kwa landa za mbao, makapi ya mpunga, majani makavu au maganda ya karanga.

Faida za ufugaji shadidi;

  • Usalama wa kuku ni kamili.
  • Huduma ya kuku ni nzuri na rahisi.
  • Ni mfumo mzuri kwenye maeneo yenye uhaba wa ardhi kwasababu huhitaji eneo dogo la kufugia.
  • Ni rahisi kutibu maradhi ya kuku.
  • Ni rahisi kudhibiti utagaji na ukusanyaji wa mayai.
  • Japo usafi ni muhmu lakini hakuna haja ya kufagia kinyesi cha kuku kila siku.
  • Faida ni ya uhakika.
  • Ni rahisi kuweka kumbukumbu.

Hasara zake;

  • Mfumo huu huhitaji gharama katika ujenzi wa banda, ulishaji wa kuku na huduma zingine za kuku.
  • Hutumia muda mwingi kuhudumia kuku zaidi ya ufugaji huria na nusu huria.
  • Kuna uwezekano wa kuku kuatamia mayai bila mpangilio kama usimamizi hautoshi.
  • Kuna uwezekano wa kuku kudonoana na kula mayai wasipokuwa na huduma na uangalizi mzuri.
  • Ugonjwa ukiingia, ni rahisi kuenea haraka.
  • Kuku watakosa mionzi ya jua ambayo ni muhimu kwa vitamin D.

Zingatia;

  • Kuku wawiane na ukubwa wa banda. Wasizidi 6 kwa kila mita moja ya mraba.
  • Banda liwe bora ambalo haliruhusu unyevunyevu na athali zingine za hali ya hewa kwa kuku.
  • Usafi wa vyombo vya kulishia unahitajika.

MAHITAJI MUHIMU KATIKA UFUGAJI WA KUKU WA ASILI

Kuku wa asili ni rahisi kufugika ila hii haimaanishi kwamba wajihudumie. Katika kufuga kwa faida, kuku wa asili huhitaji huduma madhubuti. Mahitaji makuu kwa kuku wa asili ni;

  • Makazi, chakula, chanjo na matibabu iwapo ameugua.

Hayo ndiyo mahitaji makuu na ndani ya hayo ndimo yanamo patikana mahitaji mengine.

HATUA ZA UFUGAJI WA KUKU WA ASILI KWA FAIDA

  • Kuchagua kuku bora wa kufuga.
  • Banda bora la kufugia.
  • Kutunza na kulisha kuku kulingana na hatua mbalimbali za ukuaji, na
  • Kudhibiti na kutibu magonjwa ya kuku.

KUCHAGUA KUKU BORA WA KUFUGA

Kama nilivyoeleza hapo awali, kuku wa kienyeji wapo wa aina nyingi. Ni muhimu mfugaji kuchagua kuku bora wa kuendeleza kizazi. Kuku bora wa kuendeleza kizazi hupatikana kwa uchunguzi na uchambuzi unao fanyika mara kwa mara. Sababu kubwa ya kufanya uchaguzi ni kupata kundi la kuku litakalo faa kwa sifa zote za uzalishaji. Mfugaji anatakiwa kuchagua kuku bora wa kufuga kwa kuangalia sifa zifuatazo;

  • Aina ya kuku wanao pevuka haraka.
  • Uzito mkubwa na nyama nyingi kwa umri mdogo.
  • Awe na uwezo wa kutaga mayai mengi kwa mzunguko mmoja, yasiwe chini ya 15.
  • Awe na uwezo wa kuatamia vizuri, kuangua vifaranga vingi na kuvilea.
  • Umbo kubwa na kukua haraka.
  • Uwezo wa kukabiliana na hali ya hewa na kustahilimi magonjwa.

Kuku wenye sifa nzuri ndio unao takiwa uwaache kuendeleza kizazi. Hata hivyo kuku wa asili wanaweza kuboreshwa zaidi kwa kutumia jogoo wa kisasa ili kupata kuku wanao kuwa haraka, wenye uzito mkubwa na wanao taga mayai mengi kwa mzunguko mmoja. Rhode island Red ni miongoni mwa majogoo ya kisasa yanayo pendekezwa na wataalamu wengi kutumiwa katika kuboreshea kuku wa asili.

Zoezi la ufugaji wa kuku ni kazi hivyo huhitaji muda wa kutosha. Fanya uchunguzi wa kutosha katika kuchagua kuku wa kuendeleza kizazi.

Zingatia: ni muhimu jogoo wa asili atumike kwa miaka mitatu tu ili kuepuka mchanganyiko wa damu kwa wenye nasaba moja kwani kufanya hivyo husababisha uzalishaji duni.

Uwiano mzuri wa majogoo na matetea bandani husaidia kudumisha amani ndani ya banda. Pia husaidia kupata mayai yenye mbegu ya jogoo ambayo yana uwezo wa kutoa vifaranga. Uwiano unao kubalika ni jogoo mmoja kwa tetea kumi.

BANDA BORA LA KUFUGIA

Kama kiumbe kuku huhitaji makazi bora kwa afya na usalama wake. Banda la kufugia kuku linatakiwa kuwa na ubora toshelevu. Banda bora kwa kufugia kuku ni lenye sifa zifuatazo;

  • Banda lijengwe kwenye mazingira mazuri. Iwe ni sehemu yenye mwinuko isiyotuama maji, iwe mbali kidogo na makazi ya watu, mazingira rafiki na salama kwa kuku.
  • Lenye ukubwa wa kutosheleza idadi ya kuku unao hitaji kufuga. Kila mita moja ya mraba kwa wastani wa kuku 6.
  • Pasiwe na mwelekeo wa upepo mkali
  • Liwe imara, lenye uwezo wa kuwahifadhi kuku kwa kuwakinga na athali za hali ya hewa, kama vile jua kali, mvua, baridi n.k, pia liwe lenye uwezo wa kuwakinga kuku dhidi ya wanyama hatari wanao weza kuwashambulia, kama vicheche, mwewe, kenge, mbwa, n.k.
  • Liwe na mwanga pamoja na hewa ya kutosha.
  • Liwe na paa refu linalo ruhusu mtu mzima kuingia na nafasi inayo ruhusu usafi kufanyika vizuri.
  • Liwe na sehemu ya kuwekea chakula, maji, sehemu ya kutagia, sehemu ya kuatamia, sehemu ya kulelea vifaranga na vichanja ambavyo kingo zake za juu ni za mvilingo kwaajili ya kuku kuruka na kulala.
  • Kwenye mazingira ya baridi banda liwe na ukuta mrefu unao karibia paa na sehemu ndogo inayo baki iwekwe wavu kwa ajili ya usalama wa kuku.
  • Kwenye mazingira ya joto banda liwe na ukuta mfupi na sehemu kubwa inayo baki hadi kwenye paa iwe na wavu imara kwa ajili ya usalama wa kuku.

UJENZI WA BANDA

Ujenzi wa banda hutegemeana na mazingira linapo jengwa kwa kuangalia urahisi na uwezekano wa upatikanaji wa vifaa vya ujenzi. Kwamaana hiyo, kiwango cha ubora wa banda hutegema mazingira lilipo. Banda huweza kujengwa kwa kutumia vifaa vya asili vitokanavyo na rasilimali za misitu au kujengwa kwa kutumia vifaa vya kisasa vinavyo zalishwa viwandani na wakati mwingine hujengwa kwa vifaa vya aina zote mbili kwa wakati mmoja.

Kujenga banda kwa vifaa vya asili:

Mahitaji muhimu katika ujezi wa banda kwa vifaa vya asili ni; miti (nguzo), fito, kamba za katani, mianzi au milingoti ya kuezekea, udongo wa kukandia pamoja na nyasi kwa ajili ya kuezekea paa. Ikiwa hakuna uwezekano kabisa wa kupata wavu/nyavu, tumia fito kuzifunga kwa matundu madogo sana mti/miti ya wavu ili ipatikane hewa na mwanga wa kutosha bandani. Hata hivyo bado kukiwa na uwezekano, hakikisha unasakafia chini na kuweka makapi ya mpunga au randa za mbao kama ilivyo elezwa hapo awali.

Kujenga banda kwa vifaa vya kisasa;

Vifaa vinavyo hitajika ni; wavu au nyavu za kutosha banda, tofali, mbao, simenti, misumari pamoja na mabati. Mahitaji mengine kama yakihitajika ni nondo, kokoto, mawe, n.k.

Zingatia;

Banda lolote liwe na sehemu ya kutagia, viota vya kuatamia kama unahitaji kuku wako wawe wanatamia na kutotoa vifaranga, isipokuwa banda la kuku wa nyama. Vyombo vya kulishia chakula na vyombo vya kunyweshea maji ni mahitaji muhimu bandani.

KUTUNZA NA KULISHA KUKU KULINGANA NA HATUA MBALIMBALI ZA UKUAJI

Utotoleshaji:

Hatua za maisha ya kuku huanzia kwenye yai. Hivyo basi tunaweza kusema kuwa ufugaji wa kuku huanzia kwenye yai. Yai huatamiwa kwa siku ishirini na moja kisha huanguliwa kifaranga. Utotoleshaji katika siku asili hufanywa na kuku au mashine maalumu ya kutotoleshea vifaranga.

Kuku huatamia mayai na kuyatotoa baada ya kuyaatamia kwa siku siku 21, hali kadhalika mashine huangua baada ya siku 20 – 21 tangu mayai yanapowekwa. Mashine za kutotoreshea hufanya kazi sawa na kuku japo kuna tofauti ndogo kati ya uanguaji kwa mashine na uanguaji kwa kuku. Tofauti zilizopo kati ya uanguaji kwa kuku na uwezo wa mashine ni pamoja na mashine kuwa na uwezo wa kuangua vifaranga vingi kwa wakati mmoja tofauti na kuku ambae uwezo wake ni wa kuangua vifaranga vichache.

Utotoleshaji kwa mashine

Mashine za kutotoleshea vifaranga hujulikana kwa jina la incubator. Incubator zipo za aina tofauti kufatana na muundo wake. Zipo aina mbili za mashine zinazo tumia kazi kutotoleshea, ambazo ni;

  • 1. Flat table Incubator;

Ina umbo kama meza. Flat table Incubator kwa kawaida ni ndogo na zina uwezo wa kuchukua mayai machache kati ya mayai 50 hadi mayai 500. Zina sahani kubwa za mraba ambamo huwekwa maji kwani hutumia maji ya moto au hewa yenye joto. Kati ya mashine hizo, zipo zinazotumia umeme.

  • 2. Cabinet Machine;

Hizi ni mashine kubwa zenye uwezo wa kubeba mayai zaidi ya 500. Mashine hizi hutumia umeme. Muonekano wake hufanana na sanduku au kabati. Mashine hizi hutumia feni kubwa madhufu kama Panga boi katika kuingizia na kutolea hewa. Zina namna ya kuangalia joto sahihi, hugeuza mayai na kujifekebisha zenyewe.

Utumiaji wa mashine hizi; mayai huwekwa kwenye chano za kuatamia, upande wa yai ulio chongoka kuelekea chini na upande mpana kuwa juu.

Chumba chenye mashine za kutotoleshea:

Chumba cha kuweka mashine za kutotoleshea kinatakiwa kijengwe kwa ubora unao kubalika. Kijengwe kwa matofali yaliyo tengenezwa kwa saruji pia kiwekewe sakafu imara ya saruji ili kudhibiti mabadiliko ya hali ya hewa kama vile mvua, baridi, joto na kadhalika.

Utotoleshaji wa kuku.

Kuku huatamia mayai kwa siku 21 kisha kutotoa vifaranga, hivyo basi kwa hizo siku 21 kuku apewe chakula na maji ya kutosha ili atulie asiyaache mayai kwa muda mrefu kwa ajili ya kujitafutia chakula.

Uchaguzi wa mayai kwaajili ya kutotolesha;

Siyo kila yai lina sifa ya kuanguliwa kifaranga. Uchaguzi wa mayai yafaayo kuatamisha ni moja kati ya mambo ya kuzingatia ili kupata vifaranga vya kutosha. Mayai ya kuatamisha yasiwe yamekaa siku nyingi, angalau yawe yamekaa siku zisizo zidi 20 tangu kutagwa. Mayai uliyo lenga kuatamisha yahifadhiwe vizuri katika sehemu yenye hewa ya kutosha. Yasidondokewe na maji wala yasipatwe na unyevunyevu kwa namna yoyote. Yasiwe kwenye hali ya mtikishiko, hata ukiyasafisha basi yasafishe kwa umakini yasitikisike kiasi cha kiini kuvurugika.

Mayai yafaayo kutotolesha yawe na sifa zifuatazo;

  • Yawe yaliyo rutubishwa na jogoo.
  • Yawe na ukubwa wa wastani.
  • Yasiwe na nyufa.
  • Yawe na ganda imara ambalo siyo tepetepe.

Kiota cha kuatamia;

  • Kiota kiandaliwe kabla kuku hajaanza kutaga, kiwekewe majani makavu kwa muundo wa sahani iliyo zama ndani kidogo.
  • Viota vya kuatamia viandaliwe sehemu maalumu bandani au katika chumba maalumu bandani ili kumuepusha kuku aliye atamia na fujo za kuku wengine.
  • Kiota kiwekewe dawa ya unga ya kuuwa wadudu kabla na baada ya kuweka nyasi.
  • Iwapo kuku atajiandalia kiota mwenyewe mahali panapo faa, aachiwe isipokuwa kiota kiwekewe dawa ili kudhibiti wadudu.

Dalili za kuku anaye taka kuatamia.

  1. Hapendi kuondoka kwenye kiota.
  2. Ushungi wake husinyaa.
  3. Hutoa sauti ya kuatamia.
  4. Hupenda kujikusanyia mayai mengi.

Kuku akionyesha dalili za kutaka kuatamia, kabla ya kumpa mayai, akaguliwe kwanza kama ana wadudu kama vile; viroboto, utiti, chawa n.k wanao weza kumsumbua wakati wa kuatamia. Ikiwa anao, awekewe dawa ya unga kuwadhibiti kabla ya kuatamia. Kumuacha kuku aatamie huku akiwa na wadudu, watamsumbua na kumfanya asitulie kwenye kiota hali itakayo pelekea kuangua mayai machache na megine yataharibika.

KULEA VIFARANGA

Malezi ya vifaranga hufanywa na kuku hivyo ili kulea vifaranga vizuri inabidi kuiga mfano wa kuku anavyo lea. Vifaranga huhitaji joto, chakula, maji, uangalizi na huduma zingine ili wakue vizuri. Usalama wa vifaranga huhitajika ikiwa ni pamoja na kuhakikisha hawadhuliwi na mabadiliko ya hali ya hewa, wanyama hatari kama mwewe, kunguru, kenge, vicheche n.k

Vifaranga wa asili wanaweza kulelewa na kuku au kulelewa kisasa. Iwapo umetotolesha vifaranga wengi kwa wakati mmoja, unaweza kuwaweka walelewe na kuku mmoja kati ya walio totoa, mwenye upendo kwa vifaranga, asiye na ubaguzi au ukawalea kisasa na mama zao ukawaacha huru bila vifaranga ili wawahi kutaga tena.

Kulea vifaranga wa asili kwa kuku (mama zao);

Baada ya vifaranga kutotolewa waache na mama mahali penye usalama kwa muda wa mwezi mmoja, hakikisha wanapata maji na chakula cha kutosha kila siku. Unaweza kuandaa sehemu yenye usalama kwa ajili ya kulelea vifaranga kwa kujenga banda maalumu kwa ajili ya vifaranga au kuwafunika na tenga iwapo ni wachache kwa ajili ya usalama. Vifaranga wasipigwe jua wala kunyeshewa mvua. Kama unawafunika vifaranga kwenye tenga bila mama yao, hakikisha joto ni unawarejesha kwa mama yao ili wapate kukingwa na baridi. Kwa kufanya hivi vifaranga wakifikisha umri wa mwezi mmja watenge rasmi na mama yao.

Kulea vifaranga wa asili kwa njia ya kisasa (kwa kutumia kitalu);

Kitalu kinacho zungumziwa hapa ni sehemu maalumu ya kulelea vifaranga. Andaa kitalu cha kulelea vifaranga chenye ukubwa unao endana na idadi ya vifaranga ulio nao. Kitalu kinaweza kuandaliwa ndani au nje ya banda ila kinatakiwa kuwa sehemu salama yenye kivuli, mwanga wa jua na hewa ya kutosha.

Kwa ufugaji mdogo hasa katika maeneo ya kijijini unaweza kuandaa kitalu kwa kutumia mifuko ya magunia; zungusha kuta mbili za magunia zinazo achiana nafasi ya nchi tatu katikati kisha hiyo nafasi iliyo wazi ijaze maranda ya mbao tayali utakuwa umepata kitalu cha kulelea vifaranga. Katika ufugaji mkubwa andaa kitalu/vitalu vya kudumu kwa ajili ya kulelea vifaranga. Vijengewe ukuta imara kwa kutumia tofali.

Weka taa ya chemli katikati ya kitalu ambayo itatumika kutoa joto linalo hitajika kwa ajili ya vifaranga. Pia unaweza kutumia taa ya umeme badala ya chemli. Njia nzuri na rahisi ya kulea vifaranga ni kwa kutumia taa kubwa nyekundu za umeme (wati 200 au 275) au tumia kipasha joto (Heater) Taa moja ya umeme inatosha kulea vifaranga mia moja thelathini katika sehemu za joto na vifaranga mia moja katika sehemu za baridi. Mwanzoni taa iwekwe umbali wa kati ya kitalu, Taa iendelee kushushwa karibu na vifaranga kadri baridi inavyoongezeka.

Vifaranga wakisogelea sana taa jua joto halitoshi, ongeza joto kwa kupandisha utambi wa chemli au kama ni taa ya umeme, ishushe kalibu na chemli/taa ya umeme, jua joto limezidi, punguza. Usizime chemli/taa hadi utakapoona vifaranga wametawanyika wote kwenye kitalu na kuonesha hali ya kuchangamka.

Kuku walio nyang’anywa vifaranga waludishwe kwenye kundi lenye jogoo ili wawahi kupandwa na kutaga tena. Kulea vifaranga wa asili kwa kutumia kitalu hufanya kuku waongezeke haraka.

Ili kudhibiti magonjwa vifaranga wapewe chanjo dhidi ya magonjwa yafuatayo;

  • Kideri (new castle) siku ya 3 baada ya kuanguliwa, rudia baada ya wiki tatu kisha uchanje kila baada ya miezi mitatu.
  • Kuhara damu au rangi ya ugoro (Coccidiosis) : Wapewe kinga kwa dawa ya Amprolium siku 3 mfululizo mara tu wanapofikisha umri wasiku 7 baada ya kuanguliwa.
  • Gumboro; Kuku wanashusha mbawa na kujikusanya pamoja kwa baridi, pia wanaharisha kinyesi chenye rangi nyeupe. Hutokea kuanzia wiki ya 2 hadi ya 18. Wapewe chanjo siku ya 10 hadi ya 14 baada ya kuanguliwa na rudia baada ya siku 28 na 42.

Na zingine utakazo shauriwa na mtaalamu wa mifugo wa eneo ulilopo. wapewe chakula stahiki kwa umri wao na maji safi ya kutosha wakati wote kwa muda wa miezi miwili. Baada ya hapo wanapewa chakula cha kuku wanaokua.

Kuku wakikaribia kupevuka wakiwa na miezi mitatu hadi minne tenganisha temba na majogoo ili kudhibiti kuku wenye uhusiano wa damu wasipandane wao kwa wao. Wakipandana na mayai yao yakianguliwa hawatatoka vifaranga wenye sifa nzuri. mfano: ukuaji wao utakuwa hafifu kuliko wazazi wao, uwezo mdogo kuhimili magonjwa na wengine wanaweza kuwa na ulemavu. Pia zingatia matemba hao wasipandwe na baba yao. Vilevile majogoo hao wasimpande mama yao.

ULISHAJI WA KUKU

Kama ilivyo kwa viumbe wengine, kuku pia huhitaji chakula ili waweze kuishi. Ili kuku waweze kukua vizuri, wawe na afya, watoe mazao mengi na bora wanahitaji chakula bora chenye virutubisho vyote muhimu. Chakula kinacho faa ni mchanganyiko wa viini lishe mbalimbali vyenye kazi tofauti mwilini. Kila kiini lishe hakina budi kiwe katika kiwango sahihi kulingana na mahitaji ya mwili wa kuku katika umri tofauti. Aina za vyakula vinavyo hitajika katika mwili wa kuku ni;

Protini: hupatikana katika mashudu ya karanga au alizeti, damu ya wanyama kama ng’ombe, mbuzi n.k ilivyo kaushwa, mbegu za jamii ya mikunde kama maharage, kunde soya n.k. Kazi yake mwilini mwa kuku ni kujenga mwili na kuukarabati.

Wanga: hupatikana kwenye pumba na nafaka/chenga za nafaka kama Vile: mahindi, ulezi, mtama n.k. kazi yake ni kutia nguvu mwili.

Vitamini: hupatikana kwenye majani mabichi ya mpapai, n.k. kama ni ufugaji wa nusu huria au shadidi, wape kuku wa asili majani mabichi na mabaki ya mbogamboga kila siku. Kazi zake ni; kulinda mwili na kuwezesha kuku kutaga mayai yenye kiini cha njano. Madini hususani Calsium na Fosforas: hupatikana kwenye unga wa dagaa na kwenye unga wa mifupa iliyo chomwa. Kazi yake ni kujenga mifupa na kutengeneza dawa za mayai.

Kingine cha muhimu ni maji.

Changanya chakula kiasi chochote kwa uwiano unao hitajika katika mwili wa kuku kulingana na umri wao.

Mfano wa mchanganyiko wa chakula kwa makundi mbalimbali ya kuku kwa ujazo wa kilo 100.

AINA YA CHAKULAMCHANGANYIKO KATIKA KILOGRAM KWA AJILI YA: VIFARA-NGAKUKU WANAOKUAKUKU WAZAZIKUKU WENGINE
Mahindi yaliyo barazwa.16161620
Pumba za mahindi40404050
Unga wa damu1.53
Unga wa mifupa2262
Unga wa dagaa12127
Mashudu ya Alizeti1614206
Chokaa ya mifugo812
Chumvi ya mezani0.50.50.50.5
Soya iliyobarazwa66
Egg booster2
Premix220.51
Jumla100100100100

Vyakula vingine vinavyo faa kulisha kuku ni vyenye asili zifuatazo:-

  • Mizizi: Mihogo, Magimbi na Viazi.
  • Wadudu: Mchwa, Panzi, Minyoo ya ardhini, Mende funza, Kumbikumbi n.k.
  • Matunda: Matikiti, Nyanya, Maembe, Mapapai, n.k
  • Mbogamboga, n.k.

Zingatia;

kuku wapewe maji safi ya kunywa ya kutosha muda wote. Kumpa kuku maji safi kutasaidia kudhibiti magonjwa yanayoweza kutokana na vimelea vya magonjwa vinavyo stawi katika maji yasiyo safi. Kuku wawekewe maji katika vyombo vitakavyo waruhusu kunywa bila kuyachafua.

Kuku aliyepevuka anayefugwa huria anahitaji angalau gramu 80 za chakula cha ziada kwa siku. Ni vyema chakula cha ziada kitokane na vyakula vinavyopatikana kwa urahisi katika mazingira husika na ambacho hakina ushindani na wafugaji.

Kiwango cha Ulishaji kwa Umri:

UMRI KWA WIKIKIWANGO CHA KULISHA KUKU KWA SIKU KWA(GRAM)
112 – 15
215 – 21
321 – 35
4-735 – 50
8-1555 – 60
16-65 – 80

Hakikisha wakati wote chakula cha kuku kinaandaliwa na kuhifadhiwa kikiwa kikavu (kisilowe maji) ili kisharibike kwani chakula kilichovunda kinaweza kuleta madhara kwa kuku. Pia kisitengenezwe chakula kingi kwa wakati mmoja na kukaa muda mrefu bila kutumika. Hali hiyo hufanya chakula kipoteze ubora wake.

USAFI KATIKA BANDA LA KUKU

Matandazo yanayowekwa katika sakafu ya banda la kuku hayana budi yageuzwe mara kwa mara kwa wastani wa kila baada ya miezi minne. Wakati mwingine kabla ya kipindi hiki muda wowote yanapoloana na maji. Matandazo huharakisha kukuuka kwa unyevu katika banda unaotokana na kinyesi cha kuku na pia zaidi na maji yanayomwagika. Usafi katika banda utasaidia kudhibiti kwa kiasi kikubwa magonjwa mbalimbali.

Kuokota mayai;

Usiyaache mayai ndani ya viota kwa muda mrefu, yaokote mara kwa mara ili kuepuka kuharibiwa kwa mayai hayo na kuku wenyewe. Kuku wanayo tabia ya kula mayai yao ikiwa chakula unachowapa kina upungufu wa protini. Vilevile kiasi cha mwanga unaoingia ndani ya banda kikizidi kuku hula mayai au kudonoana wenyewe kwa wenyewe. Uonapo dalili za namna hii kwenye kundi lako punguza kiasi cha mwanga kwa kuziba sehemu za madirisha.

Kama ilivyoelezwa awali kuku wapewe majani mabichi ya kutosha mara kwa mara ili wawe wanakula hayo badala ya kudonoana. Pia fuatilia kuhakikisha kama chakula kina protini ya kutosha. Kama tatizo la kudonoana na kula mayai litaendelea omba msaada kwa mtaalam wa mifugo akuelekeze jinsi ya kuwakata au kuwachoma midomo.

SURA YA 3

KUKU WA KISASA

Hawa wametokana na kuendelezwa kwa kuku wa asili. Ni kuku ambao wapo kwa ajili la kusudi maalumu ya mayai au nyama japo wengine hutumia kuku wa mayai kama nyama kwa dharura au anapoisha muda wake wa kutaga mayai. Kuku wa kisasa wapo wa aina mbili;

  1. Kuku wa mayai, na 2) Kuku wa nyama.

KUKU WA MAYAI

Hawa hufugwa kwa lengo la kupata mayai. Kwa kawaida huchukua siku 150 hadi 165 tangu kuanguliwa hadi kutaga. Mitetea hawategemei kupandwa na jogoo ili watage bali hutaga wenyewe kwa kutegemea jinsi unavyo walisha. Utagaji wao ni wa kila siku katika siku zote za kuishi kwao tangu anapoanza kutaga siku ya kwanza hadi kuzeeka isipo kuwa kama wataugua, kukosa chakula au kukosa viini lishe stahiki katika chakula. Kuku wazee wanapokoma kutaga huo hawana faida tena bali wauzwe ili kupisha wengine wachanga wawekwe ili waake na hatimae waanze kutaga.

KUKU WA NYAMA

Hawa ni kuku wanao fungwa kwa ajili ya nyama tu. Hujulikana kama Cornish crosses na wengine huwaita Cornish – bred Rocks. Ni wazuri sana kwa biashara, hukua haraka kuliko kuku wa mayai. Kuku hawa huzalishwa kwa wingi na ndio wanao tumika sana kupata nyama ya kuku katika miji mikubwa. Jina kamili (maalufu) hujulikana kama Broiler.

Broiler wana manyoya meupe na miguu ya manjano. Faida ya kuku hawa ni kupata nyama na wamesaidia sana kuziba pengo la uhaba wa nyama ya kuku wa kienyeji. Wana mwili wa kadri na ukubwa wake hutegemea ulishwaji na umri wake. Kwa kawaida kuku wa nyama huchukua siku 49 hadi 56 Tangu kuanguliwa hadi kuwa tayari kuliwa japo unaweza kumuacha zaidi ya hapo ili aongezeke zaidi ukubwa na uzito.

Tofauti kati ya kuku wa Asili na kuku wa Kisasa

Kuku wa AsiliKuku wa Kisasa
Huchukua muda mrefu kukua hadi kutaga, kuliwa au kuuzwaHuchukua muda mfupi kukua hadi kuvunwa.
Wana uwezo wa kujihudumia kwa baadhi ya huduma na kujitafutia chakula.Hutegemea mfugaji kwa huduma zote.
Ni wastahimivu wa magonjwa.Siyo wastahimivu wa magonjwa.
Huzaliana wenyewe au kuzalishwa kwa mashine.Huzalishwa kwa mashine.
Wana uwezo wa kujilinda na hatari ndogondogo.Hawana uwezo wa kujilinda.
Huhitajika mtaji mdogo kuwafuga.Huhitajika mtaji mkubwa kuwafuga.
Hula kiasiHula sana
Ni wazuri zaidi kwa afya.Hukuza uchumi haraka.
Hufugika huria, nusu huria na shadidi.Hufugika shadidi pekee.

HATUA ZA KUFUKA KUKU WA KISASA

  • Agiza vifaranga kutoka mashamba yanayoaminika.
  • Vifaranga walelewe katika chumba maalumu kilichotayarishwa mapema
  • Vifaranga wapatiwe maji safi, chakula bora na cha kutosha.
  • Daima vyombo vya maji na chakula viwe safi.
  • Chumba cha kulelea vifaranga kiwe kikavu, safi, chenye joto la wastani.
  • Mitemba ni lazima wapewe chakula maalumu ili kupata mitetea bora.
  • Mitetea wanapokaribia kutaga wapewe chakula maalumu cha kutagia na kwa kipimo maalum.
  • Chunguza kuku mara kwa mara na wale wasiotaga waondolewe.
  • Kusanya mayai mara tatu au zaidi kwa siku.
  • Kuku wa nyama lazima wapewe chakula maalumu cha kuwanenepesha (Broilers Mash).
  • Nunua chakula kutoka sehemu zinazoaminika. Endapo utatengeneza chakula mwenyewe, tengeneza chakula chenye viinilishe vyote muhimu.
  • Chukua tahadhari ya kinga na tiba dhidi ya magonjwa kwa muda unaotakiwa.
  • Tafuta soko mapema kabla ya kuuza mazao. Mazao yatayarishwe mapema kabla ya kupeleka sokoni.
  • Weka kumbukumbu zote vizuri.

SURA YA 4

UFUGAJI WA KUKU WA MAYAI

Ufugaji wa kuku wa kisasa hutofautiana na ufugaji wa kuku wa asili kwa sehemu kutokana na utofauti wao. Ufugaji wa kuku wa kisasa unahitaji utaalam zaidi ili kuwafuga kwa ufanisi. Mfumo pekee wa ufugaji unao tumika kufuga kuku wa kisasa ni mfumo Shadidi. Kuku wa kisasa hawaatamii mayai wala kuangua vifaranga hivyo uanguaji wa vifaranga wa kisasa hufanywa na mashine pekee. Mfugaji wa kuku wa kisasa anaweza kuzalisha vifaranga mwenyewe kwenye mashine au kuagiza vifaranga kutoka kwenye mashamba yanayo zalisha vifaranga.

Utumiaji wa mashine;

Mbali na maelezo niliyo elezea hapo awali juu ya utumiaji wa mashine, haya ni maelezo ya nyongeza ambayo pia ni muhimu kwa mtumiaji.

  • Mashine itumike kufuatana na maagizo ya mtengenezaji.
  • Washa mashine kwa saa 12 hadi 24 kabla hujaweka mayai.
  • Baada ya kuwasha mashine hakikisha kuwa vifaa vyote vinafanya kazi sawasawa.
  • Weka mayai kwenye mashine sehemu pana ikielekea juu.
  • Kama unatumia mashine inayofanana na meza, anza kuyageuza mayai saa 24 baada ya kuyaweka kwenye mashine. Mayai yageuzwe mara tatu kwa siku hadi kufikilia siku ya tisa.
  • Katika mashine inayofanana na sanduku au kabati mayai hayahitaji kugeuzwa kwa mkono.
  • Utambuaji wa mayai yasiyofaa kuanguliwa ufanyike baada ya siku ya tisa na ya kumi na tano katika mashine inayofanana na meza.
  • Katika mashine inayofanana na kabati, utambuaji ufanyike baada ya siku kumi na nane.
  • Mayai ya kuanguliwa yakichunguzwa kwenye mwanga baada ya siku tisa yataonyesha mishipa ya damu kando ya kiini. Hali hiyo hujitokeza zaidi baada ya siku kumi na tano na kumi na sita. Mayai yasiguswe wala mashine kufunguliwa siku tatu kabla ya kuanguliwa.
  • Baada ya siku ishirini na moja vifaranga hao watolewe kwa ungalifu ili wasipigwe na baridi wakati wa kuwahamisha kwenye sehemu ya kulelea.
  • Vifaranga wote dhaifu na waliochelewa kutotolewa hawafai kukuzwa.
  • Vifaranga wapelekwe kwenye chumba maalum kwa ajili ya kukaguliwa ili kuondoa walio na vilema, wasiokauka vitovu na manyoya. Vifaranga kwa ajili ya mayai watenganishwe na vijogoo na wapatiwe chanjo.
  • Baada ya hapo wawekwe kwenye makasha tayari kwa kuuzwa, kupelekwa kwenye sehemu ya kukuzia au kuwaingiza shambani kwao.
  • Kabla ya kuweka mayai mengine ya kuanguliwa katika mashine, ni lazima kusafisha vyano na mashine na kufukiza dawa inayopendekezwa kama vile “Potassium permangante” au Formalin 40{93c24fd6cacbcd7660749606bbfee15e2f0dc7a17fc0d61a10d1e769d752be52}.

MATAYARISHO KABLA YA VIFARANGA KUWASILI

Chumba;

Vifaranga walelewe katika chumba maalumu hadi umri wa majuma manne. Chumba kitayarishwe siku kumi na nane kabla ya vifaranga kuwasili. Matundu yote yaliyo kwenye sakafu, dari, madirisha na ukuta yazibwe. Kama chumba hicho kina sakafu ya saruji, kisafishwe kwa maji ya moto na baadaye kinyunyizie dawa kama vile Rhino au Dettol ya kuua wadudu. Ikiwa chumba hicho hakina sakafu ya saruji, toa takataka kisha mwagia chokaa. Ili kuyaweka mazingira katika hali ya usafi na kuzuia wadudu waharibifu. Mazingira yasafishwe hadi kufikia upana wa mita mbili au zaidi kuzunguka banda. Katika chumba watakamofikia vifaranga tengeneza sehemu maalum ya kulelea (Kitalu).

Vifaa vya Joto

Vifaa vya joto ni vya muhimu sana kwenye kitalu hivyo viandaliwe mapema kabla ya vifaranga kuwasili. Matumizi ya vifaa vya joto ni kama nilivyoeleza katika malezi ya vifaranga wa Asili. Aidha maelezo ya nyongeza ni:-

  • Taa ya umeme ni nzuri zaidi katika kulelea vifaranga japo ukikosa unaweza kutumia chemri au jiko la mkaa.
  • Vifaa vya joto vitumiwe kwa uangalifu ili visisababishie madhara kwenye vifaranga kwani joto likiwa dogo, vifaranga wataugua na pia likizidi wataugua ugonjwa wa joto utakao wasababishia kuanguka ovyo.
  • Mwanzoni taa iwekwe umbali wa kati ya sentimita 35 hadi 37 kutoka sakafuni Unaweza kurekebisha joto kwa kupandisha au kushusha taa.
  • Unapaswa kuwa na jiko la mkaa au taa ya chemli kwa tahadhari ya umeme kukatika.
  • Unapotumia jiko la mkaa ni lazima uhakikishe kwamba mkaa unaotumia hautoi moshi na chumba kina hewa safi na ya kutosha.
  • Weka jiko juu ya matofali ili kuzuia vifaranga wasiliguse.
  • Kama utatumia taa ya chemli, iweke juu ya matofali na izungushiwe waya ilikuzuia vifaranga wasiiguse.
  • Taa moja inatosha kutoa joto kwa vifaranga hamsini.
  • Hakikisha kwamba taa hiyo haivuji na unayo akiba ya mafuta ya kutosha.
  • Usitie mafuta mengi kwenye taa ili kuepuka kulipuka kwa taa.
  • Vifaa vya joto vianze kufanya kazi saa tatu au zaidi kabla ya vifaranga kuwasili ili chumba kipate joto la kutosha. Vile vile ni muhimu kutayarisha madawa na chakula siku moja kabla ya kuwasili vifaranga.

UAGIZAJI WA VIFARANGA

Agiza vifaranga kutoka katika mashamba au vituo vya kutotolea vifaranga vinavyotambulika. Ni muhimu mfugaji ufahamu mahali pa kupata vifaranga wa mayai au wa nyama wenye sifa zifuatazo:

  • Wawe wamekauka vizuri baada ya kuanguliwa.
  • Wawe wamepata chanjo kuzuia magonjwa mbali mbali.
  • Wasiwe na vilema au magonjwa yoyote.

MAPOKEZI YA VIFARANGA

i. Baada ya vifaranga kuwasili kutoka kwenye vituo vya kutotolea, wapelekwe moja kwa moja hadi kwenye sehemu maalumu ya kulelea.

ii. Mara tu vifaranga wakiwasili, masanduku yaingizwe ndani na yawekwe moja moja na siyo moja juu ya lingine. Vifaranga wakaguliwe, wahesabiwe na kisha wawekwe katika sehemu maalumu ya kulelea.

iii. Vifaranga wapewe maji safi, endapo watakuwa wamechoka wapewe maji yaliyochanganywa na sukari laini au glukosi kiasi cha vijiko viwili vya chakula katika lita tano za maji. Vile vile ongeza mchanganyiko wa vitamini kama vile Vitox.

iv. Baada ya saa tatu hadi nne wapewe chakula maalumu cha vifaranga.

ULISHAJI

Kuku wapewe majani mabichi laini ili kuwapatia vitamini, madini na protini, na kuzuia tabia ya kudonoana. Majani yaning’inizwe kwa kamba bandani kwa usawa utakao waruhusu kula vizuri. Hakikisha chumba ni kisafi na hakina unyevunyevu wakati wote. Unyevu husababisha ugonjwa wa baridi ambao hufanya vifaranga wajikunyate na kutetemeka na wanaweza kufa ghafla.

JOTO

Joto ni muhimu katika uhai wa vifaranga. Katika juma la kwanza joto linalostahili katika sehemu ya kulelea ni nyuzi joto 35 za Sentigredi. Joto hili hupimwa kwa kutumia kipima joto ambacho huwekwa Sentimita nne hadi tano kutoka kwenye mdara. Kiasi hiki kipunguzwe kwa nyuzi joto mbili za Sentigredi kwa kila juma hadi kufikia nyuzi joto 27 za Sentigredi katika juma la tano.

Angalia mfano katika jedwali lililopo hapa chini;

JumaJoto
135°C
233°C
331°C
429°C
527°C

Ikiwa huria kipimajoto, unashauriwa uangalie tabia na mwenendo wa vifaranga. Kama vifaranga wakichangamka wakinywa maji vizuri na kutawanyika sehemu zote, joto hilo linatosha.

Joto linalotakiwa

Kama joto halitoshi, vifaranga hujikusanya karibu na taa au hujirundika katika sehemu moja. Hivyo unashauriwa kuongeza joto kwa kuongeza idadi ya vifaa au nguvu ya joto kwa mfano umeme.

Joto Kali

Ikiwa joto ni kali sana utaona vifaranga wanakaa mbali na taa, wakipanua mabawa yao na kukihema haraka. Hali hii ikizidi huleta ugonjwa wa joto jingi, ambao husababisha vifaranga kuanguka chini. Hali hiyo ikitokea unashauriwa kupunguza idadi ya vyombo vya joto na kuwapa maji mengi ya kunywa.

Baada ya majuma manne, vifaranga watolewe kwenye sehemu maalum ya kukuzia na kupelekwa kwenye banda la kufugia. Kabla ya kuwahamisha tenganisha vijogoo kutoka kwenye kundi la vifaranga ikiwa vifaranga hivyo ni kwa ajili ya kuku wa mayai.

MALEZI YA MITEMBA NA MITETEA

Mitemba

Vifaranga wenye umri wa kuanzia majuma manne huitwa mitemba. Kuku wa umri huu wanahitaji chakula maalum cha kukuzia. Chakula hicho hupatikana katika vituo vinavyouza vyakula vya kuku, ikiwa huwezi kupata vyakula hivyo, tengeneza mwenyewe kwa kutumia aina mbali mbali za vyakula. Pamoja na kuwapa chakula, hakikisha pia unawapa maji safi na ya kutosha. Kila kuku watano hadi sita wanahitaji eneo la mraba wa mita moja. Epuka msongamano wa kuku wengi katika eneo dogo kwani msongamano husababisha vifo kutokana na upungufu wa hewa. Vile vile husababisha kuku kudumaa, kudonoana na kuchafuka kwa matandiko. Mitemba ikifikia umri wa majuma kumi na sita wawekewe viota.

Mitetea

Mitemba ikishafikia umri wa majuma kumi na nane huitwa Mitetea. Mitetea waliodumaa na majogoo waondolewe katika kundi la mitetea bora. Zuia viroboto, chawa na utitiri kwa kutumia dawa zinazoshauriwa na wataalamu. Ni muhimu kupunguza midomo ya mitetea ili wasidonoane. Mitetea hudonoana kutokana na upungufu wa protini, msongamano, mwanga mwingi na kukosa mazoezi. Ili kupunguza kudonoana ongeza protini ya asili ya nyama, ning’iniza majani mabichi, wawekee bembea ndani ya banda na ongeza nafasi ya banda kulingana na idadi ya kuku. Kama tabia ya kudonoana inaendelea punguza midomo ya juu kwa kutumia mkasi, kisu, panga au kifaa maalum. Kisu au panga liwe la moto.

Kulisha

Kuku wanapokaribia kutaga wanatakiwa wabadilishiwe chakula na kupewa chakula cha kutagia (Layers mash), badala ya chakula cha kukuzia (Growers mash). Mabadiliko hayo ya chakula yasifanyike ghafla. Changanya chakula cha kukuzia na kutagia katika uwiano ufuatao:

WikiChakula cha kukuzia.Chakula cha kutagia
183/41/4
191/21/2
201/43/4
2101

Wasipewe chakula kingi kupita kiasi kwa sababu watanenepa na hawatataga mayai ya kutosha. Chakula kidogo husababisha kuku wasitage vizuri. Inashauriwa kuongeza majani mabichi ambayo ni laini ili kuku wapate vitamini, madini na protini ya kutosha.

Utagaji na Ukusanyaji wa Mayai

Kwa kawaida kuku huanza kutaga wanapofikia umri wa majuma ishirini na mbili. Kuku wa mayai aliyetunzwa vizuri anaweza kutaga mayai zaidi ya 250 kwa mwaka, na Kuku wa mayai ana uwezo wa kutaga vizuri kwa muda wa mwaka mmoja hadi mmoja na nusu tangu anapoanza kutaga. Mfugaji achunguze kuku mara kwa mara na kuwaondoa wasiotaga.

Dalili za Kuku Wasiotaga

  • Ukiingia kwenye banda kuku huruka na kukimbia ovyo. Ukinshika ni mwepesi sana.
  • Upanga wake umekauka na kupauka.
  • Sehemu yake ya kutagia huwa kavu.
  • Kuku asiyetaga vidole vitatu haviingii kwenye nafasi iliyoko kati ya mifupa miwili ya sehemu ya kutagia.

Zingatia;

  • Ukusanyaji wa mayai ufanyike mara tatu au zaidi kwa siku ili kuzuia mayai yasichafuke, yasipasuke na kuzuia baadhi ya kuku wasiatamie na kula mayai.
  • Baada ya kipindi cha kutaga kuisha, kuku wauzwe au kutumika kwa chakula kwani utagaji wao hupungua na hula chakula kingi.

MATUNZO YA KUKU WAZAZI

Kuku wazazi ni wale wanaotaga mayai kwa ajili ya kutotolesha vifaranga. Misingi ya matunzo ya kuku hawa haitofautiani sana na ile ya kuku wa mayai isipokuwa:-

  • Hulishwa chakula kwa kiwango maalumu kila siku au kila baada ya siku moja tangu wakiwa wadogo.
  • Kuna utaratibu wa kuwapima uzito kila baada ya muda wa wiki mbili hadi tatu ili wasizidi uzito unaotakiwa.
  • Katika juma la kumi na nane kuku wazazi walishwe chakula cha kuku wazazi (Breeders mash) kama inavyoonyeshwa katika jedwali lifuatalo:-
WikiChakula cha kukuzia.Chakula cha kuku wazazi.
183/41/4
191/21/2
201/43/4
2101

Zingatia;

  • Majogoo wanafugwa sehemu tofauti na mitetea, lakini wanachanganywa na mitetea wanapofikia umri wa kuweza kupanda.
  • Uwezo wao wa kutaga mayai ni mdogo, ni chini ya mayai 200 kwa mwaka.
  • Jogoo mmoja anaweza kupanda mitetea saba hadi kumi kwa wakati mmoja.
  • Katika kundi la mitetea 7 hadi 10, kuwe na jogoo mmoja.
  • Tunza majogoo ya ziada ili yatumike endapo baadhi ya majogoo wanaotumika watapatwa na matatizo.
  • Ni muhimu kufuata maagizo ya uzalishaji.
  • Gharama ya kununua vifaranga cha kuku wazazi ni kubwa zaidi ya vifaranga wa mayai ya biashara.

SURA YA 5

UFUGAJI WA KUKU WA NYAMA

UTUNZAJI BORA WA KUKU WA NYAMA

Kuku wa nyama wana uwezo wa kukua haraka. Huwa tayari kuuzwa au kuchinjwa baada ya muda wa majuma saba hadi nane. Kuku hao huwa na uzito wa nyama usiopungua kilo moja kwa muda mfupi kuliko kuku wengine.

Matunzo ya kuku wa nyama yanafanana na ya kuku wa mayai, isipokuwa kwa tofauti hizi zifuatazo:-

  • Majogoo na majike hawatenganishwi.
  • Huhitaji nafasi ndogo kuliko kuku wa mayai.
  • Wanalishwa chakula cha kunenepesha toka siku ya kwanza.
  • Wanakula chakula usiku na mchana.
  • Mifuko 80 hadi 100 inatosheleza kuku 1000 au mifuko 8 hadi 10 kwa kuku 100 kwa majuma nane.

Faida za kufuga kuku wa nyama:

  • Hukua haraka na kuuzwa hivyo hutoa pesa haraka.
  • Hutumika kama kitoweo nyumbani.
  • Kinyesi chake hutumika kama mbolea shambani na hukuza mbogamboga haraka.
  • Manyoya yake hutumika kutengeneza maua na mito ya kulalia.
  • Huinua na kukuza uchumi wa mfugaji haraka.

KUFUKA KWA FAIDA HUHITAJI KUZINGATIA HAYA

I. Ufanye mradi wa ufugaji kuwa sehemu ya maisha yako.

II. Pata elimu na ushauri kutoka kwa wataalamu wa mifugo na kuuzingatia.

III. Usafi wa banda na mazingira ya kufugia wakati wote.

IV. Chagua kuku bora wa kuendeleza kizazi na mayai bora ya kuatamiza.

V. Zuia minyoo, utitiri na viroboto.

VI. Chanjo ya mdondo kila baada ya miezi mitatu.

VII. Chanjo ya ndui mara mbili kwa mwaka.

VIII. Tunza kumbukumbu sahihi za mradi wako.

IX. Panga kuuza kuku kwa makundi ili uongeze kipato.

X. Boresha lishe na afya ya familia kwa kula mayai na kuku.

XI. Mahesabu ya mradi yahibike, gawa mapato yatokanayo na mradi wa ufugaji kwa kuendeleza mradi, akiba na matumizi yako.

SURA YA 6

MAGONJWA YA KUKU, KINGA NA TIBA ZAKE

TAHADHALI YA KUEPUKA MAGONJWA YA KUKU KATIKA MPANGO MKAKATI WA KUANZISHA MRADI WA UFUGAJI WA KUKU.

Taratibu za kuzuia kuenea kwa Magonjwa hutekelezwa kwa lengo la kuzuia uingiaji na usambazaji wa vimelea vya ugonjwa ndani na kati ya vijiji, kaya na mashamba. Taratibu hizi ni pamoja na kuweka karantini ambapo magonjwa na vimelea vya ugonjwa huzuia kuingia katika eneo fulani, au vimelea huharibiwa na kuzuwa sehemu moja ili visipenye kuingia maeneo mengine. Hivyo basi, taratibu za kuzuia kuenea kwa magonjwa zina vipengele vikuu vitatu:

  • Karantini,
  • kudhibiti njia za usafirishaji, na
  • usafi wa maeneo.

Uandaaji wa shamba uambatane na mkakati wa kukinga/kuzuia vimelea vya magonjwa kuingia shambani. Mazingira yawe rafiki kwa kazi ya ufugaji yasiwe yenye kuruhusu uwepo na ueneaji wa vimelea vya magonjwa.

Mkakati huu uambatane na haya yafuatayo:

  • Eneo lilipo shamba au banda; Shamba au banda la kuku liwe mbali na mashamba mengine ya ndege na mifugo mingine.
  • Ni vyema banda moja likawa na kuku wa umri mmoja ili kuzuia vimelea vya magonjwa kuendelea kubaki bandani.
  • Jenga uzio ili kuzuia watu wasiohusika kuingia shambani au bandani.
  • Ramani ya shamba au mabanda upunguze pita pita za watu na uwezeshe usafi na upuliziaji wa dawa kufanyika kwa urahisi.
  • Jenga mabanda imara ambayo ndege pori na panya hawawezi kuingia.
  • Taratibu za kuendesha shughuli za shamba; Zuia kuingizwa na kuenezwa kwa magonjwa shambani kwa kudhibiti uingiaji wa watu, vyakula, vifaa, wanyama na magari ndani ya shamba.
  • Tenganisha ndege kufuatana na aina ya ndege na umri wao.
  • Weka karantini kwa ndege/kuku wapya ili wachunguzwe kwa kipindi kisichopungua wiki mbili kabla ya kuingizwa shambani au bandani.
  • Usiruhusu tabia ya kuchangia vifaa/vyombo kama vile makasha ya mayai, makreti ya kubebea kuku kati ya shamba na shamba, n.k.
  • Wafanyakazi waanze kuwahudumia kuku wenye umri mdogo kabla ya wale wenye umri mkubwa.
  • Usiruhusu watoto kucheza kwenye shamba la kuku.
  • Weka utaratibu wa kuangamiza mizoga ya kuku.
  • Anzisha programu jumuishi ya kudhibiti wadudu/wanyama waharibifu.
  • Panga utaratibu mzuri wa kuwapa kuku huduma ya maji na kufanya usafi.
  • Panga utaratibu mzuri wa kusafisha banda na kupulizia dawa.
  • Vifaa visafishwe na kuwekwa dawa ya kuua vijidudu kabla ya kuingizwa shambani.
  • Hakikisha magari yanapoingia shambani yanapita katika kidimbwi chenye dawa ya kuua vimeleavya magonjwa.
  • Hakikisha mfanyakazi anabadilisha viatu/mabuti kabla ya kuingia katika kila banda.
  • Weka taratibu nzuri za kuingia shambani, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha usafi wa viatu na mikono; au wageni na wafanyakazi kubadilisha nguo/viatu na kuvaa mabuti.

MAGONJWA YA KUKU, KINGA NA TIBA ZAKE KITAALAM

Magonjwa ya kuku yapo mengi. Hata hivyo siyo yote yanatokea mara kwa mara hapa Tanzania. Ili uweze kudhibiti yale yanayotokea katika kundi lako unahitaji kufahamu dalili za jumla za magonjwa hayo. Unapoibaini moja au zaidi ya dalili za ugonjwa au wadudu chukua hatua mara moja. Yapo magonjwa ambayo yanaweza kuangamiza kundi lote la kuku katika muda mfupi.

Jihadhari na uwezekano wa kupatwa na hasara zinazoletwa na magonjwa ambayo unaweza kuyazuia.

Zipo Dalili za Jumla za Magonjwa ya Kuku ambazo kwa kuku unaweza kuzitambua kuwa hali ya kuku wako siyo salama hata kama siyo mtaalamu au mzoefu katika ufugaji wa kuku, nazo ni;

  • Kuku kupoteza hamu ya kula.
  • Kuzubaa na kukaa mahali pamoja kwa muda mrefu (Kutochangamka).
  • Kushuka kwa kiwango cha utagaji wa mayai.
  • Vifaranga kutokua upesi au kudumaa. – Macho kuwa na rangi nyekundu.
  • Kujikunja shingo.
  • Kutetemeka, kutoa majimaji puani, mdomoni na machoni.
  • Kutoa mharo (kinyesi) wa rangi ya kijani au wenye mchanganyiko na damu au cheupe.
  • Kukonda.
  • Kukohoa.

Zionekanapo dalili hizi au moja kati ya dalili hizi katika kundi lako, chukua hatua ya kutibu haraka ili kuokoa kundi. Kama hali ni ngumu zaidi omba msaada kwa mtaalamu wa tiba ya mifugo ili achunguze mara na kushauri jambo la kufanya.

Aidha upo umuhimu katika msemo wa Kiswahili usemao kinga ni bora kuliko tiba. Njia bora ya kuwakinga kuku wako na magonjwa ni kuwapa chanjo kabla ya kuugua. Zoezi la kuchanja kuku linatakiwa kuwa endelevu tangu walipo anguliwa hadi maisha yao yote kwa utaratibu maalum ili kujiepusha na hasara zitokanazo na magonjwa au gharama kubwa za kutibu magonjwa pale yatakapotokea.

Zingatia;

Magonjwa ni changamoto na kikwazo kikubwa katika ufugaji wa kuku. Kwakuwa magonjwa mengi hatari ya kuku hayana tiba, inatakiwa kinga kufuatiliwa na kutolewa katika muda muafaka.

FAHAMU BAADHI YA MAGONJWA HATARI YASHAMBULIAYO KUKU, UENEAJI WAKE, DALILI, KINGA NA TIBA ZAKE:

Magonjwa yatokeayo mara kwa mara ni:

  • Kideri/Mdondo (New Castle Disease).
  • Ndui ya kuku (Fowl pox).
  • Kipindupindu cha Kuku (Fowl Cholera).
  • Mafua ya kuku (Infectious Coryza).
  • Homa ya matumbo (Fowl Typhoid).
  • Kuhara damu (Coccidiosis).
  • Ukosefu wa Vitamini A.
  • Minyoo na wadudu kama viroboto, chawa, utitiri na kupe wa kuku.

1. Kideri/Mdondo (New Castle Disease)

Ugonjwa huu huwapata kuku wakubwa na wadogo na ni miongoni mwa magonjwa hatari ambayo huambukizwa kwa kasi kubwa sana na kusababisha vifo. Ugonjwa huu husababishwa na virusi na huweza kushambulia pia bata, bata mzinga, kanga, kwale na ndege wengineo.

Ueneaji:

Kuku mzima kuvuta hewa yenye virusi vya ugonjwa huu toka kwa kuku mgonjwa. Upepo huweza kuhamisha virusi vya ugonjwa huu toka sehemu hadi sehemu. Watu huweza kuhamisha ugonjwa huu wanapotembea toka sehemu hadi sehemu. Kuku wasio na ugonjwa wakikaa pamoja na kuku wagonjwa. Ndege wanaokula mizoga kama kunguru huweza kusambaza mabaki ya mizoga yenye ugonjwa huu. Kuzagaa mabaki ya mifupa ya kuku aliye kuwa ameugua ugonjwa huu. Vyombo vya usafiri toka kwenye eneo lenye ugonjwa.

Dalili zake;

Homa kali, kuku kuwa dhaifu, kuzubaa na kushusha mabawa na kupoteza hamu ya kula. Kuku kupoteza fahamu na kupooza viungo, kulegea kwa shingo na inaweza kupinda kuelekea nyuma au pembeni pia huweza kuzungusha shingo. Kuhema kwa shida na hutoa majimaji mdomoni yenye harufu kali. Kukohoa, kukoroma na kupiga chafya. Kuharisha kinyesi chenye rangi ya kijani. Vifo vya mfululizo vinavyoweza kumaliza kuku wote bandani.

Matibabu ya Kideri:

  • Ugonjwa huu unaambukizwa na virusi, hivyo hauna tiba, bali isipokuwa una kinga.

Kinga ya ugonjwa:

Kuna aina mbili za chanjo ya mdondo:

A. Chanjo inayoweza kuvumilia joto (Thermostable):

Chanjo hii inaweza kutunzwa katika hali ya joto la kawaida (room temperature) na kuendelea kubaki salama kwa muda wa siku 30. Hutolewa kwa kuku kwa njia ya matone kwenye macho.

Kwa kutumia chanjo hii unaweza kuwachanja kuku muda wowote katika siku. Ila inashauriwa kuwachanja asubuhi ili kupunguza uwezekano wa chanjo kupata miale ya jua ya moja kwa moja.

Utumiaji;

  • Vifaranga wapatiwe chanjo wakiwa na siku tatu (3).
  • Kuku wasio na ugonjwa wapatiwe chanjo mapema.
  • Chanjo irudiwe kila baada ya miezi mitatu.
  • Kuku wagonjwa wauawe na mizoga yao ichomwe moto na kufukiwa.
  • Hakikisha usafi wa banda la kuku na vyombo vyote wanavyotumia.

Zingatia:

  • Usichanje kuku kama ugonjwa umeshaingia kwenye kundi.
  • Inashauriwa kuweka chanjo hii chini ya chombo kinachowekwa mtungi wa maji baridi kama hauna friji. Hii huongeza zaidi usalama wa chanjo hiyo.
  • Usiweke chanjo kwenye paa kwani joto laweza kuwa kali zaidi. Pia si vyema kubeba chanjo kwenye mifuko ya plastiki kwani hii huweza kuongeza joto zaidi.

B) Chanjo isiyovumilia joto:

Chanjo hii hutunzwa kwenye ubaridi muda wote. Hutolewa kwa kuku kwa kuchanganywa na maji ya kunywa kuku. Ikishachanganywa, huchukua muda mfupi kama wa saa moja na baada ya hapo inaanza kupoteza ubora wake. Kwa hali hiyo, inashauriwa kuwanyima kuku maji kwa muda ili wapate kiu sana na ndipo uwawekee maji ya kunywa yenye chanjo ili wayanywe kwa wingi na kwa muda mfupi. Pia inashauriwa kuwa siku ya chanjo wape kuku chakula kikavu zaidi kabla ili wapate kiu sana.

Angalizo:

  • Mdondo au kideri ni ugonjwa tishio ambao huweza kuua kuku wote.
  • Mdondo ukitokea vifo huwa vingi, kuku hupumua kwa taabu, hupooza na wengine huzunguka na kuzungusha kichwa.
  • Mdondo huweza kuzuiwa kwa chanjo kila baada ya miezi mitatu.
  • Wafugaji kuku waunde vikundi vya ushirika wa kuchanja mdondo.

2. Ndui ya kuku (Fowl Pox)

Ugonjwa huu huwashambulia kuku wadogo na wakubwa, na husababishwa na virusi.

Ueneaji:

  • Ugonjwa huu huambukizwa kwa kupitia kwenye vijeraha vya kuku.
  • Mbu na wadudu wengine waumao huweza kuambukiza anapomuuma kuku mgonjwa na halafu akamuuma kuku asiye na ugonjwa.

Dalili zake:

  • Homa kali. Kupoteza hamu ya kula. Kupungua uzito na Kutoa kamasi kwenye pua.
  • Kutokea kwa vipele sehemu mbalimbali zisizo na manyoya kisha baada ya siku kati ya 7 hadi 14 vipele hupasuka na kuacha vidonda. Mara nyingi vipele husababisha kuziba macho.
  • Vifo huweza kutokea kwa kuku wenye umri mdogo.

Matibabu:

Ugonjwa huu hauna tiba kwani huambukizwa na virusi. Ila inashauriwa kuwapa kuku dawa ya antibiotic ili kuzuia na kutibu magonjwa nyemelezi yanayoweza kuwashambulia kuku kupitia kwenye vidonda.

Kinga:

  • Ndui ya kuku huziwa kwa chanjo ya sindano.
  • Vifaranga wapatiwe chanjo wakiwa na umri wa siku arobaini na tano.
  • Tenga kuku wagonjwa na wazima.
  • Epuka madimbwi karibu na nyumbani ili kuepusha mazalia ya mbu.

Zingatia:

Ili kupunguza kasi endapo ugonjwa huu umewapata kuku, sugua majeraha au vipele kwa pamba iliyochovya kwenye dawa ya madini joto (Iodine) na baadaye paka mafuta mazito (Petroleum jelly) au samli. Hii si kutibu ugonjwa bali unawasaidia kuku kulainisha ngozi na macho yapate kuona chakula na maji.

3. Homa ya Matumbo (Fowl Typhoid)

Ugonjwa huu husababishwa na Bakteria na huwapata kuku wa umri wote. Ugonjwa huu huambukizwa kutoka kwa kuku wagonjwa kwenda kwa kuku wasio wagonjwa, kupitia kwenye mayai, chakula chenye kinyesi cha kuku wenye ugonjwa pia watu iwapo watabeba vimelea na kuja navyo kwenye banda.

Ueneaji:

  • Kuku asiye mgonjwa kula vimelea vya ugonjwa kupitia kinyesi cha kuku mgonjwa kwenye chakula.
  • Kuku mgonjwa huweza kurithisha vifaranga wake kupitia mayai aliyotaga.
  • Watu na vyombo vya usafiri wanaweza kuhamisha ugonjwa kutoka sehemu hadi sehemu.
  • Vyakula vya kuku kutoka sehemu yenye ugonjwa kwenda kusiko na ugonjwa.
  • Mizoga ya kuku yenye ugonjwa ikipelekwa sehemu isiyo na ugonjwa.

Dalili:

  • Homa kali.
  • Manyoya husimama.
  • Kinyesi kuonekana kuganda sehemu ya nyuma.
  • Kukosa hamu ya kula.
  • Kuku kudhoofika.
  • Kiwango cha utagaji hushuka.

Kinga:

  • Tenganisha vifaranga na kuku wakubwa.
  • Kuku wagonjwa watengwe na kupewa tiba ya Antibiotic.
  • Zingatia usafi wa banda na vyombo vya chakula na maji.

Matibabu:

  • Dawa aina ya Oxytetracycline (OTC) au Sulfa ambayo huchanganywa kwenye maji na kupewa kuku kwa siku 5 hadi 7.

4. Mafua ya kuku (Infectious Coryza)

Ugonjwa huu husababishwa na bakteria na hushambulia sana hasa kuku wakubwa. Bakteria hawa hupenda kuishi kwenye mavumbi.

Ueneaji:

  • Kuku asiye mgonjwa kula chakula au kuvuta hewa yenye vimelea vya ugonjwa huu.
  • Kuku wazima wanapochanganywa na wagonjwa.

Dalili:

  • Kuvimba uso chini na nyuma ya jicho.
  • Kupumua kwa shida na hata kukoroma.
  • Kuvimba kwa macho.
  • Kushindwa kula.
  • Kutokwa makamasi puani.
  • Kutoa usaha unaonuka.
  • Kuchafuka mbawa.

Matibabu:

  • Dawa za Sulfa au Antibiotic.

5. Kuhara damu (Coccidiosis)

Ugonjwa huu husababishwa na vimelea aina ya Protozoa na hushambulia kuku wote wakubwa kwa wadogo ila huathiri zaidi kuku wadogo.

Ueneaji:

  • Kuku kula chakula chenye kinyesi au maji yenye vimelea vya ugonjwa huu.

Dalili:

  • Kuharisha kinyesi kilichochanganyika na damu.
  • Kuku kudhoofu na kupungua uzito.
  • Kuku kuzubaa na kushusha mabawa.
  • Kuku kujitenga na wengine.
  • Kupoteza hamu ya kula.

Kinga:

  • Vifaranga wakifikia umri wa siku saba (7) wapewe Amprolium kwa siku tatu (3) mfululizo, hata kama dalili za ugonjwa hazijajitokeza.
  • Tenganisha vifaranga na kuku wakubwa.
  • Kuku wagonjwa watengwe na kupewa tiba haraka.
  • Zingatia usafi wa banda na vyombo vya chakula na maji.

Tiba:

Dawa aina ya Amprolium, Oxytetracycline au Sulfa ambayo huchanganywa kwenye maji na kupewa kuku kwa siku 5 hadi 7.

6. Kipindupindu cha Kuku (Fowl Cholera)

Kipindupindu cha kuku husababishwa na bakteria.

Dalili:

  • Kuharisha kinyesi cha njano.
  • Kusinzia na kulegea.
  • Kuhema kwa shida.
  • Kushindwa kusimama.
  • Kulala huku kichwa kimening’inizwa kwenye mabawa.
  • Kuwa na uvimbe kwenye mikunjo ya miguu.
  • Kutoa kamasi puani.

Kinga:

  • Chanja kuku wakiwa na umri wa miezi mitatu (3).
  • Zingatia usafi wa banda na vyombo vya chakula na maji.

Tiba:

  • Dawa aina ya Oxytetracycline (OTC) au Sulfa ambayo huchanganywa kwenye maji na kupewa kuku kwa siku 5 hadi 7.

7. Ukosefu wa Vitamini ‘A’:

Ukosefu wa vitamini ‘A’ ni tatizo la lishe ambalo huvakabili kuku kutokana na ukosefu wa chakula chenye vitamini hii. Maranyingi hujitokeza baada ya kipindi kirefu cha kiangazi kwa ajili ya ukosefu wa majani mabichi.

Dalili za kuku mwenye upungufu wa vitamini ‘A’;

  • Kuku kudumaa kutokana na kutokula vizuri.
  • Macho huvimba na kutoa uchafu mzito kama sabuni iliyolowana.

Kinga:

  • Hakikisha kuku wanapata majani ya kijani katika malisho yao. Walimie mchicha au uwanunulie na kuwapatia si chini ya mara 4 kwa wiki hasa kuku wa kienyeji.
  • Majani mabichi kutoka sehemu zenye maji.
  • Unaweza kuwapa vitamini za kuku za dukani kwa kufuata mapendekezo ya watengenezaji.

Tiba:

  • Hakuna tiba itakayomponyesha kuku baada ya dalili hizi kujitokeza na matokeo yake ni kifo.
  • kuku wote waliobakia katika banda lako wapewe dawa ya vitamini za kuku ambazo pia huwa na vitamini A kwani watakuwa na upungufu japokuwa dalili za ugonjwa hazijajitokeza.

8. Wadudu washambulia kuku

Kuku hushambuliwa na wadudu wa aina mbalimbali ambao wamegawanyika katika makundi makuu mawili kama ifuatavyo:

  • Wadudu wanaoshambulia ndani ya mwili.
  • Wadudu wanaoshambulia nje ya mwili (juu ya ngozi).

Wadudu hawa humnyonya kuku damu na kumfanya adhoofike, kupata magonjwa kwa urahisi na hatimaye kifo.

A. Wadudu washambuliao ndani ya mwili

> Minyoo:

Kuna minyoo ya aina nyingi inayoshambulia kuku na kusababisha kupungua kwa utagaji na udhoofu wa kuku. Katika minyoo yote, minyoo ya mviringo (Ascaris) hushambulia sana kuku na kusababisha madhara makubwa.

Dalili za minyoo:

  • Upungufu wa hamu ya kula.
  • Kudumaa kwa kuku wanaokua.
  • Kupungua kwa utagaji.
  • Minyoo mingine husababisha kupumua kwa shida.
  • Kuku hupungua uzito.
  • Minyoo kuonekana kwenye kinyesi.

Kinga na tiba ya minyoo:

  • Minyoo mingi hutibiwa na dawa ya Piperazine hivyo basi ni muhimu kuku kupewa dawa ya minyoo kila baada ya miezi mitatu.
  • Fanya usafi wa mabanda na kuhakikisha kwamba mabanda ya kuku hayana unyevunyevu.

B. Wadudu washamburiao kuku nje ya mwili

Hawa ni wadudu wanaokaa kwenye manyoya na ngozi. Wadudu hawa ni pamoja na Viroboto, kupe, Papasi, Chawa, Utitiri na wengineo. Wadudu hawa huwasumbua sana kuku na kuwafanya kutumia muda mwingi kujikuna na kujigaragaza kwenye vumbi badala ya kula.

  • Viroboto ni tatizo kubwa kwa vifaranga, hunyonya damu hadi kuua.
  • Utitiri hunyonya damu na huathiri sana kuku wanaoatamia.

Chanzo cha kuwepo wadudu;

  • Mipasuko sakafuni na kwenye kuta.
  • Uchafu wa mazingira uliokithiri.
  • Kuingiza kuku wageni kwenye kundi bila kuchukua tahadhari. Mfano; kununua kuku sokoni na kumuingiza bandani/kundini bila kumkagua.

Njia za kuzuia wadudu wa Nje;

  • Zingatia usafi wa banda la kuku.
  • Nyunyiza majivu au chokaa au dawa za kuua wadudu kila mara unapofanya usafi wa banda.
  • Choma masalia ya mayai yaliyoanguliwa.

Dalili:

  • Tumia dawa ya unga ya kuua wadudu kwa kuwanyunyizia kuku, kwenye viota vya kutagia na sehemu zote za banda.
  • Badilisha matandiko kila unapoona yanatakiwa kubadilishwa na uyapeleke shambani kama mbolea.
  • Kufubaa kwa manyoya.
  • Rangi ya upanga kuwa hafifu kutokana na upungufu wa damu.
  • Kukosa hamu ya chakula.
  • Ngozi kuwa nene, ngumu na yenye magamba yanayodondoka kama unga mweupe.
  • Kupungua uzito.
  • Kujikunakuna kwa kuku.
  • Wadudu kuonekana kwa macho.

Athari za wadudu washambulia kuku;

  • Kuku anayeatamia hatulii kwenye kiota, hii husababisha kutotoa vifaranga wachache.
  • Kupungua au kukoma kwa utagaji.
  • Ukuaji wa taratibu.
  • Ulaji hafifu.

Zingatia:

  • Magonjwa ni chanzo kikuu cha vifo vya kuku na hii husababisha hasara katika ufugaji, hivyo basi; hakikisha unawakinga kuku wako wa magonjwa kwa kuwachanja kila unapo fika muda wa kuwachanja kulingana na utaratibu wa chanjo utakao pewa na mtalam wa mifugo aliye karibu nawe.
  • Fanya usafi wa mabanda yako ya kuku mara kwa mara.
  • Hakikisha vyombo vya chakula na maji ni visafi.
  • Toa lishe iliyokamilika na ya kutosha.
  • Pata ushauri wa mara kwa mara kutoka kwa wataalamu wa mifugo waliopo karibu na makazi yako.
  • Kuku wageni watengwe kwa muda usiopungua siku 14 kabla hawajachanganywa na kuku wenyeji na wapewe chanjo.

KINGA NA TIBA ZA ASILI KWA MAGONJWA YA KUKU.

Mbali na dawa ulizo jifunza katika sehemu iliyo pita, pia unaweza kutumia dawa za asili zitokanazo na mimea asilia kukinga na kutibu kuku kwa magonjwa mbalimbali. Dawa za asili ni zuri zaidi kutibia kuku wa asili kuliko kuku wa kisasa kwani kuku wa kisasa wao kinga yao dhidi ya magonjwa ni ndogo na uwezo wao kuhimili magonjwa ni mdogo hivyo huhitaji dawa iliyo kwisha kuchakatwa ambavyo hufanya kazi kwenye mwili kwa haraka zaidi.

Dawa zitokanazo na mimea zinasaidia katika kukinga na kutibu maradhi mbalimbali ya kuku ni Sehemu za mimea zinaweza kuwa: Majani, Magome, Mbegu, Maua au Matunda.

Umuhimu wa kutumia dawa za asili kama kinga na tiba kwa kuku ni:

  • Hupatikana kwa urahisi, Ni rahisi kutumia, Gharama nafuu, Zinatibu vizuri, Hazina madhara.

Baadhi ya mimea inayotibu maradhi ya kuku:

> Mwarobaini (Majani, Mizizi au Magome)

  • Typhoid, Kuzuia Kideri, Kuhara, Mafua, Vidonda.

> Shubiri Mwitu (Aloe vera)

Chukua majani 3 – 5 makubwa, katakata na loweka ndani ya maji lita 10 kwa masaa 12 hadi 16. Wape kuku kwa siku 5 – 7. Dawa isiyotumika ndani ya masaa 12, mwaga na tengeneza.

Mchanganyiko huu unaweza kutibu magonjwa kama:

  • Kideri/Mdondo – Inyweshwe kabla ya kinga.
  • Homa ya matumbo (Typhoid).
  • Mafua (Coryza).
  • Kipindupindu cha kuku (Fowl Cholera).

Waone wataalamu wa mifugo ili ujifunze mafunzo yafuatayo kwa vitendo:

  • Uchanjaji wa kuku ili kuzuia maradhi.
  • Kutoa dawa ya utitiri, viroboto na chawa.
  • Namna ya kuwapa kuku dawa ya minyoo.
  • Kusafisha mabanda ya kuku kwa kutumia dawa.

> Mbarika (Nyonyo)

Dawa hii hutibu Uvimbe.

Matumizi:

  • Weka majani ya mbarika ndani ya majani ya mgomba kisha weka ndani ya jivu la moto, kisha kanda sehemu yenye uvimbe kwa kutumia majani hayo ya mbarika.

> Mlonge.

Ina vitamini A na C. Chukua majani ujazo wa mikono miwili (gao mbili). Kisha yapondeponde na kuyaweka katika lita 10 za maji na iache kwa masaa 12-16, chuja na wape kuku. Isiyotumika mwaga na tengeneza nyingine.

Mlonge hutibu:

  • Mafua.
  • Kideri/Mdondo – Inyweshwe kabla ya kinga.
  • Kipindupindu cha kuku (Fowl Cholera).
  • Homa ya matumbo
  • Ini.

> Konfrei:

  • Ina madini na vitamini nyingi.
  • Hutibu vidonda na majipu.

> Tura (Ndula/Ndulele)

  • Majani hutibu Minyoo, Matunda hutibu Vidonda.

> Papai (Majani)

Chemsha majani mawili makubwa ndani ya maji lita 6 hadi ubakie na lita 1. Poza kisha chuja.

  • Dawa hii hutibu Minyoo.

> Mwembe

Ponda Majani na chemsha ndani ya lita 6 za maji hadi ibaki lita 1. Wape kwa siku moja.

Mwembe hutibu:

  • Homa ya matumbo, Mafua, Kinga ya Kideri/Mdondo.

> Mpira

Chemsha majani au mizizi kisha uwape kuku wanywe.

Mpira hutibu: Tumbo, Vidonda na majipu.

> Minyaa (Cactus)

Hii ni aina yenye majani manene-hadi kufikia nusu nchi na mapana hadi kufikia upana wa viganja viwili vya mikono.

Minyaa hutibu Vidonda, Ngozi na Uzazi.

Angalizo:

  • Kuwa mwangalifu, Minyaa inaunguza au kubabua.

> Pilipili Kichaa

Pondaponda kiasi kisha changanya na maji na wawekee kuku wawe wanakunywa kwa muda wao.

  • Inasemekana inasaidia kutibu mdondo lakini mapema kabla ya maradhi kuingia.

> Katani

Twanga katani na kuloweka kisha wape kuku wanywe siku mbili, fanya hivyo kila baada ya miezi mitatu kwani katani ni kinga ya magonjwa mengi kwa kuku.

Pia katani hutibu:

  • Homa ya matumbo, kuhara, mafua na Vidonda.
  • Kideri/Mdondo.
  • Typhoid.

Sura ya 7

UTENGENEZAJI WA CHAKULA CHA KUKU.

Vyakula vya kuku vinaweza kupatikana madukani au kutengenezwa na mfugaji mwenyewe. Ili kuku aweze kukua haraka na kutoa mazao mengi na bora ni lazima chakula kitengenezwe katika mchanganyiko wenye uwiano mzuri uliopendekezwa. Chakula hicho lazima kiwe na viinilishe muhimu kama vile protini, wanga, madini na vitamini. Hakikisha chakula unachotengeneza kina mchanganyiko wa vyakula vifuatavyo:

  • Vyakula vya kujenga mwili kama vile jamii ya kunde, samaki, dagaa, mashudu ya ufuta, pamba na alizeti.
  • Vyakula vya kulinda na kukinga mwili usipate maradhi kama vile mafuta ya samaki na majani mabichi kama kabichi, michicha, majani ya mpapai na nyasi mbichi.
  • Vyakula vinavyojenga mifupa kama vile aina ya madini, chokaa, mifupa iliyosagwa na chumvi. Ukosefu wa vitamini na madini kama Kalsiamu na Fosforasi husababisha malege, kukunjamana kwa vidole, kufyatuka kwa misuli ya goti na kupofuka macho.
  • Maji ni muhimu sana kwani husaidia kulainisha na kurahisisha usagaji wa chakula, na kupunguza joto. Wakati wa joto kali kuku wapewe maji mengi.

Kabla ya Kutengeneza Chakula Lazima Mtengenezaji Ajue haya Yafuatayo:-

  • Jinsi ya kupata vyakula vya aina mbali mbali.
  • Kiasi cha viinilishe vinavyohitajika kwa kuzingatia umri na aina tofauti ya kuku; kwa mfano vifaranga wanahitaji protini asilimia 18 hadi 22, kuku wanaokua asilimia 17 hadi 19 na kuku wa mayai asimilimia 15 hadi 17. Vile vile madini aina ya Kalsiamu kiasi cha asilimia tatu hadi nne kinahitajika kwa kuku wa mayai na asilimia moja kwa kuku wa nyama na vifaranga.
  • Viwango vya uchanganyaji wa aina za vyakula mbali mbali. Ili mtengenezaji aweze kutengeneza chakula bora ni muhimu afuate kiwango cha uchanganyaji kilichopendekezwa. Kiasi cha aina moja ya chakula kinapozidi kinaweza kuleta madhara.

Jedwali lifuatalo linaonyesha kiwango kinachotakiwa kwa Vyakula na Viwango Vinavyohitajika katika Asilimia 100

Aina ya chakulaKiwango cha uchanganyaji ({93c24fd6cacbcd7660749606bbfee15e2f0dc7a17fc0d61a10d1e769d752be52})
VyakulaVifarangaKuku wa nyamaKuku wa Mayai
Mahindi + Pumba ya Mahindi302329
Ulezi/Mtama8
Mpunga na Pumba za Mpunga854
Ngano / Pumba za Ngano545
Mashudu ya pamba na Mashudu ya Nazi584
Mashudu ya Alizeti/Ufuta101515
Damu iliyo kaushwa555
Dagaa151515
Chokaa555
Lusina iliyo sagwa555
Chumvi0.50.50.5
Soya (Protini itokanayo na mimea)3.514.512.5
  • Kuhusu kiasi cha viinilishe kama protini, wanga, madini na vitamini vilivyomo kwenye aina za vyakula vitakavyochanganywa, Mfugaji anashauriwa amuone mtaalamu wa mifugo aliyekaribu naye aweze kumsaidia na kumpa ushauri zaidi.
  • Mchanganyiko uwe na zaidi ya aina moja ya vyakula kwa mfano vyakula vya kujenga mwili vitokanavyo na wanyama na mimea.

Mfano wa kutengeneza kilo 100 za chakula cha kuku:-

> Mfano wa chakula cha vifaranga kuanzia siku ya kwanza hadi majuma manne.

VyakulaKiasi (Kg)
Mahindi30
Pumba za mahindi20
Soya18
Mashudu ya Alizeti20.5
Dagaa5
Mifupa iliyo sagwa4
Chumvi0.5
Vitamin2
Jumla100

> Mfano wa chakula cha kukuzia kuanzia Juma la nne hadi la nane.

VyakulaKiasi (Kg)
Mahindi45
Pumba za mahindi20
Soya20
Mashudu ya Pamba5
Dagaa2.5
Mifupa iliyo sagwa5
Chumvi0.5
Vitamin2
Jumla100

> Mfano wa chakula cha kuku wa mayai kuanzia Juma la nane hadi la ishirini.

VyakulaKiasi (Kg)
Mahindi45
Pumba za mahindi25
Mifupa iliyokaushwa2.5
Soya5
Mashudu ya Alizeti10
Dagaa4
Damu iliyo kaushwa3
Chumvi0.5
Vitamin2
Chokaa3
Jumla100

Sura ya 8

KUTUNZA KUMBUKUMBU ZA MRADI WA UFUGAJI WA KUKU

Utandawazi unaendana na kumbukumbu. Kila linalo fanyika katika wakati wa sasa lazima liwe katika kumbukumbu. Kwa ufanisi wa shughuli ya ufugaji kumbukumbu ni muhimu sana katika mfugaji wa kibiashara hasa unapo lenga kufuga kwa faida kwani kumbukumbu itakusaidia kutambua kufaulu, kushindwa na udhaifu katika mradi wako.

Faida za kumbukumbu;

  • Faida au hasara inayotokana na kuendesha shughuli za ufugaji.
  • Chanjo na tiba zilizyofanyika.
  • Aina ya Magonjwa yaliyoshambulia kuku.
  • Mtindo na namna ya utendaji wa shughuli za ufugaji.
  • Kuonyesha kwa ndani namna ya shughuli ilivyoendeshwa muda uliopita au mbinu zilizotumika.
  • Maendeleo ya kuku.
  • Matukio muhimu yaliyotokea ndani ya mradi kama vile aina ya magonjwa yaliyoshambulia kuku, chanjo na tiba zilizotumika, kiwango cha utagaji wa mayai n.k.
  • Zinamuwezesha kugundua makosa na kuweka mpangilio wa masahihisho ya makosa.
  • Ni namna ya kuongeza na kuendeleza uwezo wa usimamizi wa mfugaji.
  • Huwezesha kufanya maamuzi sahihi yahusuyo mradi.

Makundi ya kumbukumbu:

  • Kumbukumbu za uzalishaji: Hizi zitamwezesha mfugaji kujua kiasi cha mayai yanayotagwa na vifaranga waliototolewa pia kujua idadi ya kuku wanaokufa kwenye banda lake hivyo aweze kuchukua tahadhari.
  • Kumbukumbu za fedha, mapato na matumizi: Husaidia kujua uwiano wa gharama za uendeshaji na mapato ili kujua kiasi cha faida inayo patikana katika mradi wako wa ufugaji.
  • Kumbukumbu za rasilimali zote katika uzalishaji: Husaidia kujua mahitaji muhimu na wakati yanapo hitajika.
  • Kumbukumbu za matibabu na kinga: Husaidia kujihami iwapo ugonjwa huo utajitokeza tena.

Utunzaji wa kumbukumbu unahitaji kufanywa kwa umakini ili kupata data sahihi na kufikia lengo. Unaweza kutumia majeduali kuandika kumbukumbu ili kuainisha mnyumbuliko.

MFANO WA MAJEDUARI YA KUMBUKUMBU

UANGUAJI VIFARANGA

TAREHE/ MWEZIIDADI YA MAYAIMAELEZO
ATAMIWA/ WEKWA MASHINENIYALIYO ANGULIWAYASIYO ANGULIWA

KALENDA YA CHANJO NA TIBA

UGONJWAMWEZI
123456789101112
GUMBORO
MDONDO
MAFUA
NDUI

IDADI YA KUKU

MWEZI/MWAKA
TAREHEIDADI YA KUKU
JOGOOTETEAVIFARANGAJUMLAMAUZO /VIFOBAKIMAELEZO
1
2
3
4

Vivyo hivyo chora majeduari ya; Kumbukumbu za uatamiaji, Mapato na matumizi na zingine zote zilizo za muhimu. Pia kumbukumbu zingine zisizohitaji jeduari ziandike kwa mfumo rahisi utakao eleweka kwa mtu yeyote atakae hitaji kuzitumia.

nitumie pdf

MWISHO.

Scroll to Top